Header Ads

FAIDA YA KUFUNGA NDOA KANISANI

Image result for faida ya kufunga ndoa ya kanisani




1, 2. (a) Nyakati nyingine tunajiuliza nini kuhusu wenzi wapya wa ndoa, na kwa nini? (b) Tutazungumzia maswali gani katika sura hii?
JE, UNAPENDA kwenda kwenye arusi? Wengi wanapenda, kwa sababu mara nyingi hizo huwa pindi zenye kufurahisha sana. Bwana na bibi-arusi wanavalia mavazi yenye kupendeza kwelikweli. Zaidi ya hilo, nyuso zao zinaonyesha kwamba wana shangwe nyingi! Siku hiyo, wana furaha nyingi na inaonekana wana matazamio mengi mazuri ya wakati ujao.
Hata hivyo, ukweli ni kwamba ndoa nyingi leo ziko mashakani. Ingawa tunawatakia mema wenzi wapya wa ndoa, nyakati nyingine tunajiuliza: ‘Je, ndoa hii itakuwa na furaha? Itadumu?’ Majibu ya maswali hayo yanategemea ikiwa mume na mke wanaamini na kutumia shauri la Mungu kuhusu ndoa. (Methali 3:5, 6) Wanahitaji kufanya hivyo ili waendelee kukaa katika upendo wa Mungu. Acheni tuchunguze majibu ya Biblia kwa maswali haya manne: Kwa nini ufunge ndoa? Ikiwa utafunga ndoa, utachagua mwenzi wa aina gani? Unaweza kujitayarisha jinsi gani kwa ajili ya ndoa? Na ni nini kinachoweza kuwasaidia wenzi wa ndoa waendelee kuwa na furaha?

KWA NINI UFUNGE NDOA?

3. Kwa nini si jambo la hekima kufunga ndoa kwa sababu ndogo-ndogo?
Watu fulani wanaamini kwamba siri ya kuwa na furaha ni kufunga ndoa na kwamba huwezi kamwe kutosheka au kuwa na furaha maishani ikiwa huna mwenzi wa ndoa. Hilo si kweli hata kidogo! Yesu, ambaye alikuwa mseja, alisema useja ni zawadi, naye aliwahimiza wale wanaoweza waupe nafasi. (Mathayo 19:11, 12) Mtume Paulo pia alizungumzia faida za useja. (1 Wakorintho 7:32-38) Hata hivyo, Yesu na Paulo hawakuweka sheria kuhusu jambo hilo; na ‘kukataza kufunga ndoa’ ni ‘fundisho la roho waovu.’ (1 Timotheo 4:1-3) Lakini wale wanaotaka kumtumikia Yehova bila kukengeushwa wanaweza kufaidika kwa kuendelea kuwa waseja. Basi, si jambo la hekima kufunga ndoa kwa sababu ndogo-ndogo, kama vile kufunga ndoa kwa sababu tu wenzako wamefunga ndoa au kwamba wanakutia moyo ufanye hivyo.
4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba ndoa nzuri huandaa mazingira yanayofaa ya kuwalea watoto?
Kwa upande mwingine, je, kuna sababu nzuri za kufunga ndoa? Ndiyo. Ndoa pia ni zawadi kutoka kwa Mungu mwenye upendo. (Mwanzo 2:18) Kwa hiyo, inatimiza mambo fulani mazuri na inaweza kuleta furaha. Kwa mfano, ndoa nzuri ndio msingi bora wa maisha ya familia. Watoto wanahitaji kulelewa katika mazingira yanayofaa wakiwa na wazazi wanaowapenda, wanaowatia nidhamu, na kuwapa mwongozo. (Zaburi 127:3; Waefeso 6:1-4) Hata hivyo, kusudi la ndoa si kupata na kulea watoto tu.
5, 6. (a) Kulingana na Mhubiri 4:9-12, urafiki wa karibu una faida gani? (b) Ndoa inaweza kuwa kama kamba yenye nyuzi tatu jinsi gani?
Fikiria andiko la msingi la sura hii pamoja na mistari inayotangulia: “Wawili ni afadhali kuliko mmoja, kwa maana wana thawabu nzuri kwa ajili ya kazi yao ngumu. Kwa maana mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake. Lakini itakuwaje kwa yule aliye peke yake akianguka wakati ambapo hakuna mwingine wa kumwinua? Tena, wawili wakilala pamoja, watapata joto; lakini aliye peke yake anawezaje kupata joto? Na mtu akiweza kumshinda nguvu mmoja aliye peke yake, wawili wakiwa pamoja wataweza kusimama dhidi yake. Nayo kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.”—Mhubiri 4:9-12.
Andiko hilo linazungumzia hasa faida ya urafiki. Bila shaka, ndoa ni muungano wa marafiki wa karibu zaidi. Kama andiko hilo linavyoonyesha, katika muungano huo wenzi wa ndoa wanaweza kupata msaada, faraja, na ulinzi. Ili kifungo cha ndoa kiwe imara zaidi, mengi zaidi yanahitajika. Kamba yenye nyuzi mbili, kama mstari huo unavyodokeza, inaweza kukatika. Lakini kamba yenye nyuzi tatu zilizosokotwa au kufumwa pamoja haikatiki kwa urahisi. Lengo kuu la mume na mke linapokuwa kumpendeza Yehova, ndoa yao ni kama kamba yenye nyuzi tatu. Kwa kuwa Yehova anahusishwa kabisa, ndoa hiyo inakuwa muungano imara sana.
7, 8. (a) Paulo aliwapa shauri gani Wakristo ambao hawajafunga ndoa wanaopambana na tamaa za ngono? (b) Biblia inatusaidia jinsi gani kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu ndoa?
Pia, katika ndoa ndipo tu tamaa za ngono zinaweza kutoshelezwa inavyofaa. Ni katika kifungo hicho tu ambapo mahusiano ya kingono huonwa kwa kufaa kuwa chanzo cha shangwe. (Methali 5:18) Hata baada ya mtu kupita kipindi ambacho Biblia inakiita “upeo wa ujana”—wakati ambapo tamaa za ngono huanza kuwaka—huenda bado akahitaji kuzuia tamaa hizo. Zisipozuiliwa, tamaa hizo zinaweza kumwingiza katika mwenendo mchafu au usiofaa. Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuwapa watu ambao hawajafunga ndoa shauri hili: “Ikiwa hawawezi kujizuia, acheni wafunge ndoa, kwa maana ni bora kufunga ndoa kuliko kuwaka tamaa.”—1 Wakorintho 7:9, 36; Yakobo 1:15.
Hata kuwe na sababu gani za kufunga ndoa, mtu anapaswa kuona mambo kihalisi. Kama Paulo alivyosema, wale wanaofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Wakorintho 7:28) Watu waliofunga ndoa hupata matatizo fulani ambayo waseja hawapati. Hata hivyo, ukiamua kufunga ndoa, unaweza kufanya nini ili upunguze matatizo na kuwa na furaha zaidi? Njia moja ni kuchagua mwenzi wa ndoa kwa hekima.

KUCHAGUA MWENZI WA NDOA ANAYEFAA

9, 10. (a) Paulo alionyesha jinsi gani hatari ya kuwa na urafiki wa karibu pamoja na wasioamini? (b) Mara nyingi kupuuza shauri la Mungu la kutofunga ndoa na mtu asiyeamini huwa na matokeo gani?
Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kanuni ya maana ambayo mtu anapaswa kutumia anapochagua mwenzi wa ndoa: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.” (2 Wakorintho 6:14) Mfano aliotumia unatokana na maisha ya ukulima. Wanyama wawili wanaotofautiana sana kwa ukubwa au nguvu wakifungwa nira pamoja, wote wawili wataumia. Vivyo hivyo, mwamini na mtu asiyeamini wanapofungwa nira pamoja katika ndoa, bila shaka watakwaruzana na kugongana-gongana. Ikiwa mmoja wao anataka kuendelea kukaa katika upendo wa Yehova naye yule mwingine hajali hata kidogo, mambo wanayotanguliza maishani yatatofautiana na huenda hilo likatokeza mkazo mwingi. Hivyo, Paulo aliwasihi Wakristo wafunge ndoa “katika Bwana tu.”—1 Wakorintho 7:39.
10 Nyakati nyingine, Wakristo fulani ambao hawajafunga ndoa wanaona kwamba ni afadhali kufungwa nira isivyo sawa kuliko kuishi maisha ya upweke. Wengine wanaamua kupuuza shauri la Biblia na kufunga ndoa na mtu ambaye hamtumikii Yehova. Mara nyingi matokeo yamekuwa yenye kusikitisha. Watu hao hujikuta wamefunga ndoa na mtu ambaye hawawezi kuzungumza pamoja naye mambo ya maana zaidi maishani. Wanakuwa wapweke hata zaidi kuliko walivyokuwa kabla ya kufunga ndoa. Inafurahisha kwamba kuna maelfu ya Wakristo waseja wanaotegemea na kushikamana na mashauri ya Mungu kuhusu jambo hilo. (Zaburi 32:8) Ingawa wanatarajia kwamba siku moja watafunga ndoa, wanaendelea kuwa waseja mpaka watakapopata mwenzi kati ya wale wanaomwabudu Yehova Mungu.
11. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuchagua mwenzi wa ndoa kwa hekima? (Ona pia sanduku “Ninatafuta Mwenzi wa Aina Gani?”)
11 Hata hivyo, haimaanishi kwamba kila mtumishi wa Yehova anaweza kuwa mwenzi wa ndoa anayefaa. Ikiwa unafikiria kufunga ndoa, tafuta mtu ambaye utu na miradi yake ya kiroho inapatana na yako, na anampenda Mungu kama wewe. Jamii ya mtumwa mwaminifu imechapisha habari nyingi kuhusu jambo hilo, na ingefaa ufikirie kwa uzito na kusali kuhusu mashauri hayo ya Kimaandiko, na kuwa tayari kuongozwa nayo unapofanya uamuzi huo muhimu.*Zaburi 119:105.
12. Ni desturi gani kuhusu ndoa inayofuatwa katika nchi nyingi, na ni mfano gani wa Biblia unaotoa mwongozo?
12 Katika nchi nyingi, wazazi humchagulia mtoto wao mwenzi. Kulingana na utamaduni wa watu katika maeneo hayo, wazazi huonwa kuwa wana hekima na uzoefu mwingi zaidi ambao unahitajiwa ili kufanya uamuzi huo wa maana. Mara nyingi ndoa hizo zinafaulu, kama ilivyokuwa nyakati za Biblia. Mfano wa Abrahamu wa kumtuma mtumishi wake akamtafutie Isaka mke unaweza kuwasaidia wazazi walio katika hali kama hiyo leo. Abrahamu hakuhangaikia pesa wala umaarufu. Badala yake, alifanya juu chini kumtafutia Isaka mke kati ya watu wanaomwabudu Yehova.*Mwanzo 24:3, 67.

KUJITAYARISHIA NDOA YENYE MAFANIKIO

13-15. (a) Kanuni iliyo katika Methali 24:27 inaweza kumsaidia jinsi gani mwanamume anayefikiria kufunga ndoa? (b) Mwanamke anaweza kufanya nini ili kujitayarisha kwa ajili ya ndoa?
13 Ikiwa unafikiria kwa uzito kufunga ndoa, unapaswa kujiuliza, ‘Niko tayari kweli?’ Jibu la swali hilo halitegemei tu maoni yako kuhusu upendo, ngono, kuwa na mwenzi, au kulea watoto. Badala yake, kuna miradi hususa ambayo kila mwanamume au mwanamke anayetaka kufunga ndoa anapaswa kufikiria.
14 Mwanamume anayetafuta mke anapaswa kufikiria kwa uzito kanuni hii: “Tayarisha kazi yako huko nje, uifanye tayari kwa ajili yako shambani. Kisha ujenge nyumba yako.” (Methali 24:27) Andiko hilo linamaanisha nini? Katika siku hizo, mwanamume alipotaka ‘kujenga nyumba yake’ au kuwa na familia kwa kufunga ndoa, alipaswa kujiuliza, ‘Ninaweza kumtunza na kumtegemeza mke na watoto wowote tunaoweza kuwapata baadaye?’ Kwanza alipaswa kufanya kazi, atunze mashamba au mazao yake. Kanuni hiyohiyo inatumika leo. Mwanamume anayetaka kuoa anapaswa kujitayarisha kwa ajili ya majukumu ya ndoa. Maadamu afya yake inamruhusu, ana wajibu wa kufanya kazi. Neno la Mungu linaonyesha kwamba mtu ambaye haandalii familia yake mahitaji ya kimwili, kihisia, na kiroho ni mbaya kuliko asiye na imani!—1 Timotheo 5:8.
15 Vivyo hivyo, mwanamke anayeamua kuolewa anakubali kuchukua majukumu mazito. Biblia inataja stadi na sifa ambazo mke anahitaji anapomsaidia mume wake na anapoitunza familia yake. (Methali 31:10-31) Wanaume na wanawake wanaokimbilia maisha ya ndoa bila kuwa tayari kwa ajili ya majukumu yanayohusika ni wenye ubinafsi, nao hawafikirii wanachoweza kuchangia katika ndoa. Zaidi ya yote, wale wanaofikiria kufunga ndoa wanahitaji kujitayarisha kiroho.
16, 17. Wale wanaopanga kufunga ndoa wanapaswa kufikiria kwa uzito kanuni gani za Maandiko?
16 Kujitayarisha kwa ajili ya ndoa kunatia ndani kufikiria kwa uzito majukumu ambayo Mungu amempa mume na mke. Mwanamume anapaswa kujua maana ya kuwa kichwa katika familia ya Kikristo. Jukumu hilo si leseni ya kupiga ubwana. Badala yake, lazima amwige Yesu katika kuutumia ukichwa. (Waefeso 5:23) Vivyo hivyo, mwanamke Mkristo anapaswa kuelewa jukumu lake lenye heshima akiwa mke. Je, yuko tayari kujitiisha chini ya “sheria ya mume wake”? (Waroma 7:2) Tayari yuko chini ya sheria ya Yehova na ya Kristo. (Wagalatia 6:2) Mamlaka ya mume wake katika familia ni sheria nyingine. Je, anaweza kuunga mkono na kutii mamlaka ya mwanamume asiye mkamilifu? Ikiwa hayuko tayari kufanya hivyo, afadhali asiolewe.
17 Zaidi ya hilo, kila mmoja anapaswa kuwa tayari kutosheleza mahitaji ya pekee ya mwenzi wake wa ndoa. (Wafilipi 2:4) Paulo aliandika: “Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” Akiongozwa na roho ya Mungu, Paulo alitambua kwamba mwanamume ana uhitaji wa pekee wa kuhisi kwamba mke wake anamheshimu sana. Naye mke ana uhitaji wa pekee wa kuhisi kwamba mume wake anampenda.—Waefeso 5:21-33.
Wakati wa uchumba, wachumba wengi hutenda kwa hekima kwa kuambatana na mtu mwingine katika matembezi yao
18. Kwa nini wachumba wanapaswa kuonyesha sifa ya kujizuia wakati wa uchumba?
18 Kwa hiyo basi, uchumba si kipindi cha kujifurahisha tu. Ni wakati wa mwanamume na mwanamke kujifunza kutendeana inavyofaa na kuona ikiwa wanafaana kwa ajili ya ndoa. Pia ni wakati wa kuonyesha sifa ya kujizuia! Kupita mipaka katika kuonyeshana mahaba kunaweza kuwa kishawishi chenye nguvu sana, kwa kuwa kila mmoja anavutiwa na mwenzake. Hata hivyo, wale wanaopendana kikweli wataepuka matendo yoyote yanayoweza kuharibu uhusiano wa mpendwa wao pamoja na Mungu. (1 Wathesalonike 4:6) Kwa hiyo, ikiwa una uchumba, onyesha sifa ya kujizuia; sifa hiyo inaweza kukusaidia katika maisha yako yote, iwe utafunga ndoa au hapana.

UNAWEZA KUFANYA NINI ILI NDOA IDUMU?

19, 20. Toa mfano unaoonyesha jinsi maoni ya Mkristo kuhusu ndoa yanavyopaswa kutofautiana na maoni ya watu wengi ulimwenguni leo.
19 Ikiwa wenzi wanataka ndoa yao idumu, wanapaswa kuwa na maoni yanayofaa kuhusu uwajibikaji. Mara nyingi sinema na vitabu vya hadithi huisha watu wawili wanaopendana wakifunga ndoa na kuishi raha mustarehe, maisha ambayo wengi hutamani sana. Lakini, katika maisha halisi, ndoa si mwisho bali ni mwanzo—mwanzo wa kitu ambacho Yehova alitaka kidumu. (Mwanzo 2:24) Kwa kusikitisha, watu wengi ulimwenguni leo hawana maoni hayo. Watu fulani hulinganisha kufunga ndoa na “kufunga pingu za.” Huenda wasitambue jinsi hilo linavyofafanua vizuri maoni ya wengi leo kuhusu ndoa. Namna gani? Ingawa pingu zinaweza kufunga kitu kwa nguvu kwa muda unaohitajika, zinaweza pia kufunguliwa kwa urahisi.
20 Wengi leo huona ndoa kuwa ya muda tu. Wanaingia katika ndoa haraka-haraka kwa kuwa wanafikiri itatosheleza mahitaji yao, lakini wanatazamia kwamba watatoka kwa urahisi mambo yakichacha. Hata hivyo, kumbuka kwamba Biblia inapozungumzia kifungo, kama vile kifungo cha ndoa, inatumia mfano wa kamba. Kamba za meli hukusudiwa kudumu, zisikatike-katike wala kufumuka hata kunapokuwa na dhoruba kali sana. Vivyo hivyo, ndoa imekusudiwa kudumu. Kumbuka kwamba Yesu alisema: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mathayo 19:6) Ukifunga ndoa, unapaswa kuwa na maoni hayohayo kuhusu ndoa. Je, uwajibikaji wa aina hiyo huifanya ndoa iwe mzigo? Hapana.
21. Mume au mke anapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mwenzi wake, na ni nini kinachoweza kuwasaidia kufanya hivyo?
21 Kila mmoja anapaswa kuendelea kuwa na maoni yanayofaa kuhusu mwenzi wake wa ndoa. Kila mmoja wao akifanya yote awezayo kukazia fikira sifa nzuri na bidii ya mwenzake, ndoa hiyo itakuwa yenye furaha na yenye kuburudisha. Je, kuwa na maoni yanayofaa kuhusu mwenzi asiye mkamilifu ni kujifanya kipofu? Yehova hawezi kamwe kuwa kipofu, hata hivyo, sisi hutazamia awe na maoni yanayofaa kutuelekea. Mtunga-zaburi alisema: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Waume na wake pia wanapaswa kuwa na maoni yanayofaa na kuwa tayari kuwasamehe wenzi wao wa ndoa.—Wakolosai 3:13.
22, 23. Abrahamu na Sara waliweka mfano gani mzuri kwa wenzi wa ndoa leo?
22 Kadiri miaka inavyopita, ndoa inaweza kuwa baraka hata zaidi. Biblia inazungumzia ndoa ya Abrahamu na Sara walipokuwa wazee. Bila shaka maisha yao yalikuwa na mabonde na milima. Wazia hali ya Sara. Huenda alikuwa na umri wa miaka 60 na kitu alipoondoka makao yake yenye starehe katika jiji lenye ufanisi la Uru na kwenda kuishi katika mahema maisha yake yote. Hata hivyo, alijitiisha chini ya ukichwa wa mume wake. Alikuwa kikamilisho na msaidizi kwelikweli kwa Abrahamu, na kwa heshima alimsaidia kufanikisha maamuzi yake. Ujitiisho wake haukuwa wa kijuujuu. Hata “ndani yake mwenyewe,” alimwita mume wake bwana. (Mwanzo 18:12; 1 Petro 3:6) Alimheshimu Abrahamu kutoka moyoni.
23 Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba Abrahamu na Sara walikubaliana katika kila jambo. Siku moja alitoa pendekezo ambalo “halikumpendeza Abrahamu hata kidogo.” Lakini Abrahamu alitii maagizo ya Yehova, na kwa unyenyekevu akaisikiliza sauti ya mke wake, nayo familia yao ikabarikiwa. (Mwanzo 21:9-13) Waume na wake leo, hata wale ambao wamekuwa katika kifungo cha ndoa kwa miaka mingi, wanaweza kujifunza mengi kutokana na wenzi hao wenye kumwogopa Mungu.
24. Ni ndoa za aina gani zinazomletea heshima Yehova Mungu, na kwa nini?
24 Katika kutaniko la Kikristo, kuna maelfu ya ndoa zenye furaha—ambamo mke anamheshimu sana mume wake, mume anampenda na kumstahi mke wake, na wote wawili wanatanguliza mapenzi ya Yehova maishani mwao. Ukiamua kufunga ndoa, chagua mwenzi wa ndoa kwa hekima, jitayarishe vizuri kwa ajili ya ndoa, na ufanye yote uwezayo kuwa na ndoa yenye amani na upendo ambayo inamletea heshima Yehova Mungu. Ukifanya hivyo, ndoa yako itakusaidia kukaa katika upendo wa Mungu.
Ona sura ya 2 ya kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
Katika taifa la Israeli, watu fulani waaminifu walikuwa na wake wengi. Ingawa Yehova hakuanzisha zoea hilo, aliliruhusu, naye alitoa mwongozo ambao ungefuatwa katika ndoa za aina hiyo. Hata hivyo, Wakristo wanajua kwamba Yehova haruhusu tena waabudu wake wawe na wake wengi.—Mathayo 19:9; 1 Timotheo 3:2.

No comments