Header Ads


Marekani imechukua hatua isiyo ya kawaida na kuwaita Maseneta wote kwa kikao cha kupashwa habari kuhusu Korea Kaskazini katika ikulu ya White House.
Washington imeendelea kueleza wasiwasi wake kuhusu mpango wa Korea Kaskazini kuendelea kufanya majaribio ya makombora na silaha za nyuklia, na vitisho vyake kwa majirani zake na Marekani.
Kikao hicho, ambacho kitashirikisha maseneta 100 pamoja na waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Rex Tillerson na Waziri wa Ulinzi James Mattis kitafanyika Jumatano.
China, mshirika mkuu wa Korea Kaskazini, imehimiza pande zote kuwa na uvumilivu.

Rais wa China Xi Jinping alitoa wito huo alipozungumza kwa simu na Rais Donald Trump Jumapili.
Bw Xi alihimiza pande zote mbili "kuvumiliana na kujiepusha na vitendo ambavyo vinaweza vikaongeza wasiwasi zaidi", kwa mujibu wa wizara ya mambo ya nje ya China.
Kwa upande wake, bw Trump amesema Korea Kaskazini inahatarisha uthabiti katika rasi ya Korea kwa kuendelea na msimamo wake mkali.
Haki miliki ya picha AFP
Image caption Mwenyekiti wa Jopo la Wakuu wa Majeshi ya Marekani Joseph Dunford atakuwa miongoni mwa watakaowapasha habari Maseneta.
Maafisa wa Ikulu ya White House mara kwa mara huwapasha habari wabunge kuhusu masuala ya usalama, lakini ni nadra sana kwa bunge lote la Seneti kwenda White House.
Pamoja na Bw Tillerson na Jenerali Mattis, kutakuwepo pia na Mkuu wa Taifa wa Ujasusi Dan Coats na Jenerali Joseph Dunford, Mwenyekiti wa Jopo la Wakuu wa Majeshi ya Marekani.
Msemaji wa ikulu ya White House Sean Spicer alipoulizwa maswali kuhusu kikao hicho aliwaomba wanahabari waelekeze maswali yao kwa kiongozi wa wengi katika bunge la Seneti, Mitch McConnell.
Wasaidizi wakuu wa Rais Trump ambao walihojiwa na Reuters, walisema Bunge la Wawakilishi pia linataka kuandaliwe kikao sawa na hicho cha maseneta kuhusu Korea kaskazini.
Washington imesema kundi la meli za kivita, likiongozwa na meli kubwa yenye uwezo wa kubeba ndege USS Carl Vinson, linatarajiwa kufika rasi ya Korea siku chache zijazo.
Hii ni licha yakuwepo na habari za utata kuhusu zilikokuwa zinaelekea meli hizo awali.
Meli hizo za kivita vilikuwa zimedaiwa kuwa njiani kuelekea rasi ya Korea zikitokea Australia lakini baadaye zikaelekea hadi mlango wa kuingia Bahari ya Hindi.
Lakini sasa maafisa wa jeshi la wanamaji la Marekani wamethibitisha kwamba meli hizo zinaelekea rasi ya Korea.
Bw Trump pia ameambia mabalozi wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwenye mkutano White House kwamba Umoja wa Mataifa ni sharti uiwekee Korea Kaskazini vikwazo vipya.

Gazeti la chama tawala cha Workers' Party Rodong Sinmun alieleza meli hiyo kuwa "mnayama".
Korea Kaskazini imeahidi kuendelea na majaribio yake ya makombora licha ya onyo la Bw Trump na wataalamu wanasema kwamba taifa hilo linajiandaa kufanya jaribio jingine la silaha ya nyuklia.
Washington ina wasiwasi kwamba Pyongyang inaweza kupata uwezo wa kuweka bomu la nyuklia kwenye kombora linaloweza kuifikia Marekani.
China inahofia uwezekano wa kuzuka kwa vita kamili rasi ya Korea, ambavyo vinaweza kusababisha kusambaratika kwa utawala wa Kim Jong-un.
China ina wasiwasi kwamba tukio kama hilo linaweza kupelekea wakimbizi wengi kukimbilia usalama China. Aidha, uwepo wa Wamarekani Korea Kaskazini utaifanya Marekani kuwa na udhibiti wa eneo linalopakana na China.

No comments