Header Ads

Ajifungua salama watoto wanne

Mkazi wa Kijiji cha Isengule kilichopo katika mwambao wa Ziwa Tanganyika, wilayani Tanganyika, Mkoa wa Katavi, Fatuma Issa (22) aliyejifungua watoto wanne kwa mara moja (kulia) akiwa amebeba mtoto wake hao huku wengine wakijuliwa hali na Mkuu wa Wilaya ya Mpanda, Lilian Matinga katika Wodi ya Wazazi ya Hospitali ya Manispaa ya Mpanda mkoani humo. (Picha na Peti Siyame)

MKAZI wa Kijiji cha Isengule kilichopo mwambao mwa Ziwa Tanganyika katika wilayani Tanganyika mkoani Katavi, Fatuma Issa (22) amejifungua salama watoto wanne kwa njia ya kawaida katika Hospitali ya Manispaa ya Mpanda mwishoni mwa wiki.
Muuguzi Mkuu wa hospitali hiyo, Alexanda Kasagula, mama huyo aliyejifungua pamoja, watoto wake wana afya njema.
“Mtoto wa kwanza ambaye ni wa kike alizaliwa akiwa na uzito wa kilo moja na gramu 800, mtoto wa pili alizaliwa akiwa na uzito wa kilo moja na gramu 500, wa tatu alizaliwa akiwa na uzito wa kilo moja na gramu 800 huku wa nne alizaliwa akiwa na kilo moja na gramu 700.
“Kati ya watoto hao, wa tatu ni wa kiume, hali ya mzazi na watoto wake wote wanaendelea vizuri bado wamelazwa katika wodi ya wazazi hospitalini hapa,” alieleza Kasagula.
Mama huyo aliwaeleza kuwa uzao huo ni wa tatu kwake na mumewe Augustino Andrew (25) na kwamba sasa wanakuwa na watoto watano.
“Mie na mume wangu sasa tuna idadi ya watoto watano, uzazi wangu wa kwanza nilizaa mtoto mmoja ambaye yuko hai. Hii itakuwa mara yangu ya pili kujifungua watoto zaidi ya mmoja katika uzao wangu wa pili nilijifungua pacha, lakini mmoja wao alikufa muda mfupi baada ya kuzaliwa na pacha mwenzake alikufa miezi mitatu baada ya kuzaliwa…”.
“Na sasa nimejifungua watoto wanne, lakini tangu nijifungue sijapata tatizo lolote la kiafya, naendelea vizuri na watoto wangu wote. Nawashukuru wauguzi walionisaidia hadi nimejifungua salama,” alieleza mama huyo na kuongeza kuwa mama yake mzazi ndiye anayemwangalia hospitalini hapo.
Kaimu Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dk Jafar Kitambwa alisema mama huyo na watoto wake wataendelea kuwa chini ya uangalizi hospitalini hapo.


Wengine ninyi ni MALOFA   Mchungaji Lusekelo kwa Waumini wake


No comments