Header Ads

WAZIRI wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako amesema hadi sasa wizara hiyo haina deni

WAZIRI wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako amesema hadi sasa wizara hiyo haina deni inayodaiwa na walimu nchini na kwamba madeni yaliyokuwepo ya Sh bilioni 22 yalishalipwa.






Profesa Ndalichako alisema hayo juzi jioni wakati akizungumza kwenye kipindi cha Tunatekeleza kinachorushwa hewani moja kwa moja na Kituo cha Televisheni cha Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC1).
Akizungumzia madeni ya walimu, alisema serikali inawajali walimu nchini na zipo jitihada mbalimbali zimekuwa zikifanywa kuhakikisha madai yao yanahakikiwa na kulipwa ili kuepuka malimbikizo.
Alisema madeni ya walimu yako ya aina mbili; moja ni madeni ya mishahara ambayo wao wizara hawayashughulikii bali yapo chini ya Ofisi ya Rais, Utumishi na kwamba madai aina ya pili ni yale yasiyo na mshahara kama vile likizo, matibabu na mengineyo, ambayo yako chini ya wizara yake na hadi sasa wameshalipa Sh bilioni 22 na hakuna madeni mengine kutoka kwa walimu na kuwataka walimu nchini kama wana madeni mapya kuanzia sasa wayawasilishe wizarani kwa ajili ya kuhakikiwa na kulipwa.
“Wizara tunatambua mchango wa walimu na umuhimu wao kwa upande wetu, hatuna madai yoyote ya walimu yale yanayotuhusu, kwa sababu huwa tuna utaratibu wa kulipa kadri tunavyoyapata na kama yapo kwa sasa wayalete, fedha za kulipa zipo,” alisema Profesa Ndalichako.
Akizungumzia suala la watumishi hewa, Profesa Ndalichako alisema ni vyema walioguswa katika uhakiki huo unaoendelea kufanywa na timu ya watendaji kutoka taasisi mbalimbali, wakiwemo wakurugenzi, wakajiondoa wenyewe kwenye ajira kwa sababu mashtaka yanawangoja.
Kuhusu uhakiki wa wanafunzi wa elimu ya juu, Profesa Ndalichako alisema hadi sasa wamekamilisha uhakiki wa vyuo 31 kati ya vyuo 80 vilivyopo nchini na wameshabaini wanafunzi hewa 2,921 ambao hawakujitokeza wakati wa uhakiki, licha ya matangazo na msisitizo kutolewa.
Profesa Ndalichako alisema wakati kazi ya uhakiki ilipoanza, walitoa matangazo katika vyuo vyote na pia vyuo navyo vilitoa matangazo kwenye mbao za matangazo vyuoni na pia kupitia vyombo vya habari na pia kupitia serikali ya wanafunzi katika vyuo husika, lakini idadi hiyo haikujitokeza kuhakikiwa.
Alisema kwa wale wachache waliopuuza kuhakikiwa hata kama wako mwaka wa mwisho wa masomo, bado watatambulika kama wanafunzi hewa hadi pale watakapohakikiwa na hiyo itawagharimu kulipa gharama za kufanyiwa uhakiki huo.
Akizungumzia changamoto za wanafunzi kutojua kusoma na kuandika, Profesa Ndalichako alisema serikali imekuwa imetoa mafunzo kwa walimu wanaofundisha darasa la kwanza na la pili na kwamba kadri muda unavyosonga ndivyo tatizo linavyoondoka.
Kuhusu utaratibu wa utoaji mikopo kwa elimu ya juu, Profesa Ndalichako alisema changamoto zipo kutokana na mfumo uliokuwa ukitumika, lakini hatua zimeshaanza kuchukuliwa ili kuuboresha ili kuhifadhi kumbukumbu za wanufaika ili iwe rahisi kuzidai.
Aidha, alisisitiza wanafunzi waliomaliza shahada zao katika vyuo mbalimbali nchini na ikagundulika kuwa walizipata kwa njia ya rushwa, ikibainika watanyang’anywa.

No comments