Header Ads

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amewaomba viongozi wa dini zote kutumia nyumba za ibada, kuhamasisha

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amewaomba viongozi wa dini zote kutumia nyumba za ibada, kuhamasisha waumini wao umuhimu wa kulinda na kudumisha amani na utulivu uliopo nchini.





Amesisitiza kuwa Serikali itadumisha amani na utulivu nchini kwa nguvu zote ili Watanzania wawe na uhakika wa kuendelea kufanya kazi zao za kuwaingizia kipato na kuwaletea tija. Waziri Mkuu alisema hayo wakati akizungumza na waumini wa dini ya Kiislamu baada ya kumaliza swala ya Idd el Haji kwenye viwanja vya Mwembe Yanga, Temeke Dar es Salaam jana. Akizungumza kwenye Baraza la Idd alisema;
"Serikali itaendelea kuimarisha ulinzi katika maeneo yote nchini. Wito wangu kwa viongozi wa dini msisitize waumini juu ya utunzaji wa amani pamoja na kukemea vitendo viovu ili Taifa lizidi kusonga mbele".
Majaliwa aliwasisitiza wananchi kuendelea kuwaombea mahujaji waliopo Makka na Madina nchini Saudi Arabia, wakiendelea na Ibada ya Hija warudi salama.
Pia Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo, kuwaomba wananchi kuwasaidia kwa hali na mali watu waliokumbwa na tetemeko la ardhi mkoani Kagera, ambako jumla ya watu 16 walikufa, wengine 253 kujeruhiwa na maelfu ya wananchi kukosa makazi baada ya nyumba 840 kuanguka na nyingine 1,264 kupata nyufa, yakiwemo majengo 44 ya taasisi mbalimbali za umma.
Awali, akisoma hotuba ya Idd viwanjani hapo, Mhadhiri wa Kimataifa, Shehe Nurdin Kishki alisema Uislamu ni dini ya amani, hivyo amewaomba waislamu kujiepusha na vitendo vya uvunjifu wa amani yakiwemo mauaji ya watu wasiokuwa na hatia. Shehe Kishki alisema ni muhimu watu kulinda amani, kwani ikitoweka ni vigumu kuirudisha.
Alitoa mfano wa nchi za Libya na Misri, ambazo hadi sasa zimeshindwa kuirudisha. Alisema mtu yeyote anayejihusisha na vitendo vya umwagaji wa damu, kudhulumu mali za watu na kuwavunjia heshima wenzake, atakuwa ameangamia, hivyo aliwataka Watanzania hususan wakazi wa Temeke kujiepusha navyo.
"Temeke sasa inaongoza kwa matukio ya mauaji, wanaua hadi walinzi. Askari wameuawa bila hatia, jambo hili linasikitisha sana. Watu waliokuwa wanafanya kazi ya kulinda raia na mali zao wanauawa bila ya hatia,” alizungumza kwa masikitiko na kuwaomba Watanzania wajiepushe na vitendo hivyo.Pia Shehe Kishiki aliipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuonesha dhamira ya dhati ya kuwatumikia wananchi na kuwaletea maendeleo hivyo aliwaomba wananchi wawe mstari wa mbele kutoa ushirikiano ili taifa liweze kusomba mbele.
"Ndugu zangu tumepewa heshima kubwa leo kuswali Idd na Waziri Mkuu, tena amekuja hapa kwenye viwanja hivi vya Mwembe Yanga, hii inaonesha ukaribu wa viongozi wetu wakuu kwa wananchi wao hususan wa hali ya chini," alisema.
Bakwata yalia na weledi wa viongozi
Katika hatua nyingine, Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), limewataka waislamu kubadilika kwa kufanya mambo kulingana na taaluma ili kuepuka viongozi wenye mmomonyoko wa maadili na wasiojitambua.
Mufti wa Tanzania, Shehe Mkuu Abubakar Zuberi aliyasema hayo jana baada ya swala ya Idd katika Makao Makuu ya baraza hilo, Kindononi, iliyofuatiwa na Baraza la Idd lililohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali. Mufti alisema wakati umefika kwa Waislamu kubadilika, kwani wapo wanaofanya kazi kinyume na taaluma zao.
Pia alisema baraza hilo linatarajia kufungua vituo vya kutoa elimu ya kuongeza maarifa 'Nyumba ya maarifa', lengo likiwa ni kuongeza ujuzi na maarifa ya elimu ya dini katika jamii na nchi. "Uwepo wa vituo hivi utasaidia kutoa ujinga na kuwa na viongozi bora kutokana na elimu ya nafasi fulani aliyosoma na kujua kuishi na watu, awali Bakwata haikuwahi kuwa na vituo vyake vya dini vinavyojitegemea," alisema.

No comments