Header Ads

KUVUA SAMAKI MWISHO MWEZI HUU

KUVUA SAMAKI MWISHO MWEZI HUU


WAZIRI wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dk Charles Tizeba, amesema kuanzia Desemba mwaka huu, meli zinazopewa leseni kwa ajili ya kuvua samaki katika ukanda maalumu wa bahari zitaanza kushusha samaki katika Bandari ya Dares Salaam.
Alisema hayo jijini Dar es Salaam mara baada ya kutembelea bandari hiyo ili kuona uwezekano wa meli hizo kupata eneo la kushusha samaki.
“Maandalizi yanaendelea kwa ajili ya meli hizo kuweza kupata eneo la kushushia samaki, tumefika hapa kuona mamlaka zimejipangaje katika suala hili, kwani tumekuwa tukipoteza mazao hayo yatokanayo na samaki kwa muda mrefu,” alisema Dk Tizeba.
Alisema serikali imesimamisha leseni kwa ajili ya meli zinazovua ili zitakazopewa zipate mahali pa kushushia. Alisema jambo hilo litasaidia samaki kuongezeka mtaani na kuwezesha wananchi wengi kununua huku bandari nayo ikinufaika.
Alisema moja ya masharti ambayohupewa meli hizo wakati wa kupatiwa leseni ni kushusha samaki waliovuliwa kinyume cha leseni zao, lakini walikuwa wakilalamika kukosa mahali pa kuwashusha.
“Leseni wanazopewa wavuvi hao wenye meli ni kuvua aina moja ya samaki, lakini pindi wanapokamata samaki wengine wanatakiwa kuwaleta, ni jambo ambalo limekuwa halifanyiki kwa madai kuwa wanakosa mahali pa kushushia huku wananchi wa Tanzania wakishindwa kunufaika,” alisema na kuongeza kuwa bei za samaki katika maeneo mbalimbali ni za hatari sana.
Kaimu Meneja wa Bandari, Nelson Mlali, alisema ifikapo Desemba meli hizo zitaweza kushusha samaki hao na tayari wamewaonesha wahusika vifaa na maeneo mbalimbali yatakayohusika kwa muda pamoja na uratibu mzima wa kuhifadhi samaki hao pindi watakaposhushwa.

No comments