Header Ads

Ukuta mrefu unaozunguuka machimbo ya madini ya Tanzanite katika eneo la Mererani nchini Tanzania, umekamilika kwa zaidi ya asilimia 90
"Waanze kujenga ukuta eneo hilo lote na kazi hii ifanyike haraka, watakapojenga ukuta wataweka kamera na patakuwa na mlango mmoja ambapo patajengwa vifaa maalum, nataka niwaeleze ukweli ndugu zangu wa Simanjiro hata kama utameza Tanzanite itaonekana" Agizo la Rais Magufuli mwaka uliopita

Ukuta mrefu unaozunguuka machimbo ya madini ya Tanzanite katika eneo la Mererani nchini Tanzania, umekamilika kwa zaidi ya asilimia 90.
Ukuta huo wenye urefu wa kilomita 24.5 na urefu wa mita tatu kwenda juu, umejengwa kufuatia agizo lililotolewa na Rais John Magufuli, kama jitihada za kudhibiti na kuzuia utoroshwaji wa madini hayo, ambayo yanapatikana nchini Tanzania pekee.
Tayari wakuu wa vyombo vya usalama, wametembelea eneo hilo, kuukagua ukuta huo uliojengwa kwa gharama za kiTanzania isiyozidi bilioni 6.
Na kusisitiza kuwa lengo la kujengwa kwake ni kuzuia uhalifu na si kuwazuia wachimbaji wakubwa na wadogo kupata riziki zao.

Ukuta wote mpaka sasa umegharimu shilingi bilioni 6 za Kitanzania

Wakitoa taarifa kwa viongozi wa ulinzi, wataalamu waliojenga ukuta huo, wanasema licha ya kufanikisha ujenzi huo, changamoto mbalimbali walikutana nazo ikiwemo hatari inayo ukabili ukuta huo, kutokana na wachimbaji kulipua baruti, karibu na ukuta, hivyo kusababisha hatari za kuharibika haraka.
Kwa upande wao, wakizungumzia usalama baada ya kukagua eneo hilo, wamezungumzia uadilifu katika kulinda eneo hilo.
Mkuu wa Majeshi Venance Mabeyo amesema ukuta uko imara na kwamba hatua ya pili itafuata katika kuuboresha zaidi.
Amesisitiza kuwa ulinzi unahitaji uzalendo zaidi kutokana na Watanzania wakati mwingine kuwa ndio wanaohujumu mali za nchi.
Naye Mkuu wa Jeshi la Polisi Simon Siro amesema jambo kubwa ni wananchi kuwa na uelewa kwa nini ukuta huo umejengwa.
Baada ya kukamilika kwa awamu hiyo ya ujenzi, awamu ya pili itafuata kuboresha baadhi ya maeneo na kuweka vifaa zaidi vya kiusalama.
Rais wa Tanzania John Magufuli anatarajiwa kuuzindua rasmi ukuta huo, utakapokamilika kwa asilimia mia moja.

No comments