Header Ads

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan leo ameanza ziara ya siku nne




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan leo ameanza ziara ya siku nne mkoani Iringa ikiwa na lengo la kuhamasisha shughuli mbalimbali za maendeleo na kuzindua mradi wa kuendeleza utalii ukanda wa kusini mwa Tanzania – REGROW.
Mara baada ya kuwasili mkoani Iringa , Makamu wa Rais alifungua wodi mpya katika Zahanati ya Kising’a ambapo aliwaomba wananchi wote wajiunge na mfuko wa Bima ya Afya ili waweze kunufaika na huduma bora za afya.
“Niwaombe sana ndugu zangu kila mmoja ahakikishe ana bima ya afya, bima ya afya ndio mkombozi wako, unapopata mavuno yako weka pesa ya bima ya afya, alisema”.
Makamu wa Rais alitoa pongezi kwa Wananchi hao kwa mwamko wa kuchangia ujenzi na kutoa eneo lakini pia pongezi kwa umoja wa makampuni ya Asas kwa ufadhili wa shilingi za kitanzania milioni 125.
Makamu wa Rais alisema Ilani ya CCM inaagiza kujenga zahanati katika kila kijiji hivyo ujenzi wa Wodi hii katika Zahanati ya Kising’a ni utekelezaji wa maagizo ya Ilani hiyo.
Makamu wa Rais aliwataka wananchi kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa ukimwi kwani unapoteza nguvu kazi ya Taifa kwani mpaka sasa wastani wa maambukizo umeongezeka mpaka kufikia asiliamia 22.3 kwa mwaka 2016/17 toka asilimia 9.1 mwaka 2011/ 2012.
Wakati huo huo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan alitembelea kiwanda cha Ivori Food & Bevarage na kujionea namna kiwanda hicho kinavyozalisha bidhaa zake kwa kutumia malighafi kutoka ndani ya nchi ikiwemo Cocoa toka Kyela,Nyanya toka Ilula, mahindi toka kwa wakulima wa Iringa, Rukwa na Ruvuma.
Aidha Makamu wa Rais alitembelea kampuni ya GBRI Business Solutions inayozalisha bidhaa za mboga mboga za EatFresh na kuzungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo Bi. Hadija Jabir



No comments